Saturday, October 22, 2011

ELIMU YAKO NI IPI?

Hayati Mwl. J.K Nyerere


Elimu ni nini?
Elimu na fedha/kipato
Je elimu yako ni ipi?
 Je umefata nini shule?
 Je uta/umetoka na nini shule?
Je umejiandaa kupata ajira?
 Je umejiaandaa kutengeneza ajira/kujiajiri?
Kumkichwa ni wewe!

Elimu ni nini?

Ni wimbo mzuri wa wasanii, ni wosia muhimu wa wazazi kwa watoto wao katika maono yao, ni utunzi mzuri wa muswada wa tamthiliya katika tasnia ya ugizaji, ni uwanja mzuri wa wachezaji uwanjani, ni upendo wa dhati kwa wapendanao kwa dhati, ni shairi zuri na tamu kwa watunzi bora wa mashairi, ni kilio kikali cha waliozembea uzuri huu na pia ni mti mzuri wenye matunda matamu kwa wale waliotilia maanani kote duniani katika kuutafuta utamu huu. "Elimu".

Elimu ni ufunguo wa maisha, Elimu ni mwanga, Elimu ni bahari, Elimu ni nguzo ya maisha na wazee wetu hutusisitiza kwa kusema “Elimu ni urithi wenu”.

Baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema “Elimu ni kitu cha kumkuza binadamu tu na kumwezesha kupanua uwezo wake ili anawiri”.

"Elimu ni kitu cha kumsaidia binadamu katika mapambano ya maisha. Kupambana na mazingira yanayomzuia binadamu kustawi/kuendelea katika kutaka binadamu huyu afikie hali yake ya mwisho".  

Mwenyezi mungu anatuambia katika vitabu vitakatifu “itawaleni dunia”, “itafute elimu ili muitawale dunia, muitawale namna ambayo mtaweza kuendelea”.

Sasa kama mazingira yanamzuia binadamu kutawala dunia, elimu inatakiwa itumike katika kuondoa vikwazo hivyo ili binadamu aweze kufikia utukufu wake wa kuitawala dunia. Kwa hiyo lengo la elimu sio lingine bali kuondoa vikwazo vyote na matatizo yote yanayomsumbua binadamu kufikia malengo yake/utukufu wake.
Kuna watu wamekua wakiniuliza "Kumkichwa, Umuhimu wa elimu ni upi? Upo wapi? Nisipokua na elimu je nitafanikiwa? Je mbona wako wenye elimu lakini hawajafanikiwa?" kwa upande wangu niliona kuwa hayo ni baadhi ya maswali ambayo binadamu wengi hupenda kujiuliza na kuuliza watu kama kigezo cha kuipenda ama kutaka kuitafuta elimu, pia kama kigezo cha kutoipenda elimu na kutotaka kujishughilisha katika kuitafuta elimu. nikaamua nitafute maana ya maneno haya. Ujinga na Elimu.

Ujinga ni nini? Ni hali ya kutokua na ufahamu wa jambo au kitu Fulani. Mjinga ni mtu asiye na ufahamu na jambo lilivyo ama kitu Fulani namna kilivyo.

Elimu ni ujuzi unaoupata au ni taaluma unayoipata ili kuongeza uelewa na kupanua fikra zako kama binadamu.

Elimu na fedha/kipato

Katika uchunguzi wangu nimebaini kuwa watu wengi huchanganya elimu na kipato.Ni kosa kuchanganya elimu na fedha/kipato. Tofauti kati ya uwezo wa elimu na uwezo wa fedha ni mkubwa kwani uwezo wa kifedha/kipato unatokana na njia unazotumia kutafuta kipato. Tofauti nyingine ni kwamba kwa kutumia Elimu unaweza ukajifunza mbinu za kutengeneza njia za kupata fedha kwakua fedha hazitafutwi bali zinatengenezewa njia ya kuzipata. Sasa elimu yetu isiwe ya kutafuta fedha/kipato bali ya kutengeneza njia za kuingiza kipato na pia kutumia fedha hizo katika kutuletea maendeleo. Pia tofauti  nyingine ni kwamba fedha zinaweza kutumika katika kuitafuta elimu. Hivyo fedha na elimu vinaweza kutegemeana ingawa tunatakiwa tuvitofautishe katika kuvitafuta na katika kuangalia mafanikio ya mtu kielimu na kifedha.

Elimu yako ni ipi?

 Ni ya kufundishwa darasani ama ya kujifunza mwenyewe. Kuna mkanganyiko ambao uko katika fikra zetu hasa za vijana ama wanafunzi walio katika kuitafuta elimu. Elimu sio tu ile unayofundishwa shuleni/darasani. Kuna elimu tunayoipata kila siku katika maisha yako ya kila siku. Kwa mfano ni nani aliyekuambia ukujisikia halifulani mwilini mwako ni njaa, ni ugonjwa, ni baridi. Kuna elimu tunaipata bila kwenda shule. Ifuatayo ni baadhi ya mifano ya Hayati Mwl. JK Nyerere niliyoipata kwenye baadhi ya vitabu vyake nilivyovichambua na hotuba zake ili kuweza kuandika makala hii.

Mfano wa kwanza: Ni nani aliyegundua kua binadamu anaweza kusafiri juu ya maji, atakua alianza kwa kuweka ubao juu ya maji, kisha akagundua kua ubao unaweza kuelea, vipi ubao huu ukiwa chombo, chombo hiki lazima kiwe na nafasi katikati ili chombo kielee, kisha makasia yakamsumbua, akagundua kuna upepo, lazima tuusome upepo tuujue unaendaje, akagundua kitambaa, akaunda mtumbwi. Hapa akatengeneza njia ya kusafiria baharini. Hii ni Elimu.

Mfano wa pili: Ni nani aliyegundua kua samaki hawezi kukamatwa kwa mkono lazima tutafute kitu cha kumkamatia, akagundua ndowano, ila akajiuliza bila kitu cha kumvutia samaki huwezi kumkamata samaki kirahisi, akagundua tuweke kinyama juu yake, kisha samaki atakuja kutaka kukila. Hapo umetengeneza njia ya kumkamata samaki. Hii ni Elimu.

Mfano wa tatu: Ukienda milima ya Pare kule utakuta barabara kwenye milima, ukiuliza hizi barabara mmezitengenezaje?, watasema “kabla ya barabara kulikua ni miamba mikubwa sana, ila tulitafuta njia ya kuipasua miamba hiyo na tukaipata, tulikua tunawasha moto juu ya mwamba kisha kabla mwamba huo haijapoa tunaumwagia maji ya baridi kisha unapasuka wenyewe. Hii ni elimu kabla ya uvumbuzi wa baruti.

Mfano wa mwisho wa baba wa taifa ni ugunduzi wa ndege. Binadamu katika kukabiliana na mazingira yake akaona mbona ndege wanaruka? Kwanini sisi tusiruke? Binadamu hawa hawa wakajiuliza maswali, wakajaribu kukabiliana na mazingira yao, kisha wakagundua na kutengeneza ndege. Leo tunaruka na Concode. Ndege inatoka London kuja Nairobi kwa muda wa saa tatu. Kisha binadamu akaenda mwezini. Yote hii ni elimu.

Kwa kutumia mifano ya sasa (2011)kuna wagunduzi kama Steve Jobs (Apple) Bill Gates (Microsoft), Mark Elliot Zuckerberg (Facebook). Kivipi watu hawa wameweza kukabiliana na mazingira yao?, Je ni elimu ndio imewawezesha?. Je ni elimu ipi? Jiulize ni elimu ipi? Wote hawa hawakumaliza chuo! waliacha kabla ya kumaliza chuo. Waligundua njia za kuingiza kipato baada ya kupata elimu ya kukabiliana mazingira yao. Vipi wewe elimu yako ni ipi/ yakutafuta fedha ama yakutengeneza njia za kuingiza fedha. Tusitafute Elimu ili tukatafute fedha ila tutafute elimu ili tutengeneze njia za kuingiza fedha/kipato.  Elimu yako iwe ya kukabiliana na mazingira yako yanayokunyima kuyatawala. Jifunze ugundue, pambana na mazingira, yasome uyafahamu, endelea usikate tamaa, vikwazo ndio tunavyovitafuta ili tuvitatue, elimu yetu ni kuvishinda vikwazo vyetu vinavyotunyima kuendelea.
     
Je umefata nini shule?

Hembu kumbuka wakati unataka kwenda shule huwa unawaaga wazazi, walezi, ndugu, jamaa na marafiki zako kwamba “nakwenda shule”. Na wao wanajua kuwa unakwenda shule, na wewe unajua kua unakwenda shule. Je unakwenda kufanya nini? Je wanafikiria unakwenda kufanya nini? Je unafikiria unakwenda kufanya nini? Fikra ni moja tu ni kujifunza. Je ukishajifunza nini kinafuata? Kwanini  umekwenda kujifunza? Ili iweje? Je shule ni kifungo? Je ni mahali pakwenda kujifunza kucheza? Je ulienda ili kujifunza kupunguza usumbufu nyumbani? Hapana au ndio? Jiulize kwanini ulienda shule kujifunza? Je ulifuata mafunzo ya nini?

Kumbuka kufungua macho sio kuamka, kunyanyua mguu sio kutembea, ila kujua unapokwenda ndio mwanzo wa kujifunza. Je unajua unapokwenda? Dr. Ernesto Che Guevara alisema “ni bora kufa na fikra zinazoishi kuliko kuishi na fikra zilizokufa” kwanini uishi na firka zilizokufa, kwa ninavyojua mahali unapopajua ni karibu kuliko mahali usipopajua, sasa kwanini usiende unapopajua, na kwanini usijifunze usipopajua ili upajue kisha pawe karibu, jifunze ugundue, gundua uendelee.

Kwenda shule ni kikwazo cha kwa kwanza, cha pili kujifunza, cha tatu ni kugundua ulichojifunza kwa kukielewa, cha nne ni kuitumia elimu uliyopata kwa kuelewa ulichojifunza na kuleta maendeleo kwa kuondoa vikwazo vinavyokukabili. Vikwazo hivi vyote ukivitatua basi ujue umepata elimu kwani umeweza kukabiliana na mazingira yanayokunyima kuendelea.

Je umetoka na nini shuleni?

                Kuna vitu wasomi wanaviheshimu sana, vitu hivi vinaitwa Vyeti, elimu yako iko kwenye vyeti, je ni kweli elimu yako iko kwenye vyeti? Hapana au Ndio? Elimu sio vyeti, vyeti ni tahakiki tu kuthibitisha kua ulipata elimu. Kinachotakiwa ijiulize ni “umepata nini kwenye elimu yako uliyoitafuta shuleni/chuo?” Iko wapi, mbona hatuoni mabadiliko kwako na kwa jamii yako kama kweli vyeti vyako vinaonesha umepata elimu. Umejifunza nini? Je umetoka na nini? Katika mambo yanayotunyima maendeleo ni kutokujua kua tumetoka na nini shuleni na tunatakiwa tuitumieje elimu tuliyoipata shuleni! Vyeti vinaonesha umefaulu lakini wewe tukikutazama hauna ufaulu wowote. Kwanza umekua mharibifu kwa elimu uliyopata. Elimu yako hiyo imekua ya prestige.

                Baba wa taifa alisema “Actually watu wengi wanatafuta elimu kutafuta a lot of prestige, basically kitu kinachotoa prestige ni kitu ambacho ni cha wachache. Elimu ya prestige is nonsense kwa sababu inamfunga mwingine”. Alisisitiza kuwa tusitafute elimu ili kupata heshima, eti kwakua kuna ambao hawana elimu basi ujenge tabaka la wewe mwenye elimu na wao wasio na elimu. Tuipige vita elimu ya sifa. Umuhimu wetu ni katika kuunganisha jamii yetu na kuiletea maendeleo kwa kutumia elimu tuliyoipata. Na ndicho tunachotakiwa tutoke nacho shuleni/chuoni. Mbinu mbadala za kujikomboa wewe na za kuikomboa jamii yako kutokana na mazingira yanayowazuia kupata maendeleo.

Je umejiandaa kupata ajira au umejiaandaa kutengeneza ajira/kujiajiri?
             
           Kuna jambo ambalo limekua kasumba kwa wanaosoma chuoni, na kwa tuliomaliza elimu ya juu mwaka huu wa 2011“Ajira”, ajira ya kujiajiari ama ya kuajiariwa? Jiulize kwanini uajiriwe, pia jiulize kwanini ujiajiri? Naomba nitilie mkazo katika ajira iwe kuajiriwa ama kujiajiri hasa kwa wenzangu waliohitimu elimu ya juu. “Kazi ni kazi” tusichague sana kazi. Fanya kazi yoyote kwakua nayo ni kazi. Ila ningependa tujifunze mbinu za kujitengenezea ajira kuliko kujifunza kusubiria kuajiriwa. Tusome ili tufahamu mbinu za kutengeneza ajira, tutengeneze njia za kutuingizia kipato. Katika watu wenye mafanikio wengi wao ni waliojiajiri tofauti sana na walioajiriwa wanaosubiria mafao ya uzeeni. Ukiajiriwa unapata usalama(security), ndio hiyo ni sawa ila vipi kama ukianzisha biashara yako au miradi yako kisha ukawapa watu fursa ya kukutengenezea kipato na wao kujitengenezea vipato vyao. Tuwe wabunifu, hakuna wengine kama sisi, huu muda ndio wetu. Kumkichwa ni wewe
              
                  Kuna wenye uwezo wa kuona karibu na wenye uwezo wa kuona mbali, kuna wenye uwezo wa kuona ndani ya sanduku na wenye uwezo wa kuona nje ya sanduku. Sasa kuna wale wenye uwezo wakuona vitu tofauti na wengine wanavyoviona.  Kama watu hawa wapo sasa nini kifanyike. Ushirikiano katika kufanya mabadiliko kwa jamii zetu zisizo na uwezo kama wakwetu. Usiwe mbinafsi katika kutumia ulichonacho, kitoe watu wakione, kitumie kubadilisha hali ya maisha ilivyo. Kuna wanaoona nafasi ya kufanya jambo, kuna wanaoweza kutumia nafasi watakapoambiwa ipo, kuna watakaokamilisha nafasi kwakua imeshaonekana na imeshafanyiwa kazi. Wote hawa watafanikiwa kama watashirikiana. Chamuhimu tushirikiane kwa kua kila mmoja ana upeo tofauti na wengine. Umoja wetu ndio nguvu yetu. Tupige vita ubinafsi. Nanukuu kwa kusema "Maendeleo ni mtoto wa ushirikiano".
                
               Hivyo maisha  ni mapambano, maisha ni vita, katika mapambano yoyote kunaweza kukawa na mapinduzi. Hayati Mwl. J.K Nyerere alisema “ Fanyeni kazi kwa ajili ya Mapinduzi, Msiogope Mapinduzi”. Mwalimu alituhimiza Vijana na Wanafunzi wa Tanzania “kufikiri, kuuliza maswali na kuchambua mambo”.  Kumkichwa ni wewe baada ya kuyasoma haya sasa yazingatie ili uweze kuona utofauti wa elimu uliyoipata na elimu uliyoikosa au unayoikosa na elimu unayotakiwa uitafute. Ningependa kuwashauri vijana wenzangu kusoma vitabu vingi kwa wingi ili wapate ufahamu wa mambo ili wawe huru na ili waweze kuchambua, kufikiri na kuuliza maswali. Kumbuka kumkichwa ni wewe!

No comments:

Post a Comment